Bodaboda 20 wakamatwa na Polisi Dar kwa tuhuma za kushambulia kwa mawe Basi la Mwendokasi

Jeshi la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam linawashikilia madereva 20 wa bodaboda kwa tuhuma za kulishambulia na kuliharibu basi la mwendokasi.

Wanadaiwa kulishambulia basi hilo baada ya mwenzao kugongwa na kufariki dunia.

Akizungumza jana Jumanne Desemba 11, 2018 Kamanda wa Kanda hiyo, Lazaro Mambosasa alisema Desemba 8, saa nane usiku eneo la Manzese Tiptop, dereva bodaboda akiwa anapita katika barabara ya mwendokasi aliligonga basi hilo na kusababisha vifo vya watu wawili.

Alisema watu wawili waliokuwa wamepanda bodaboda hiyo walifariki dunia pamoja na aliyekuwa akiendesha.

Alisema baada ya ajali hiyo madereva hao wanaoegesha pikipiki zao kando ya barabara hiyo walianza kulishambulia basi hilo kwa mawe na kusababisha uharibifu.

Mambosasa ametoa onyo kwa madereva wote wa vyombo vya moto hususan pikipiki kuacha mara moja kutumia barabara za mabasi ya mwendokasi ili kuepusha ajali ambazo zinagharimu maisha ya watu.


from MPEKUZI

Comments