Hukumu ya Tido Mhando Kusomwa Disemba 18

Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam Desemba 18 itatoa hukumu ya kesi inayomkabili aliyekuwa mkurugenzi mkuu wa Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC), Tido Mhando.

Tido ameshtakiwa kwa matumizi mabaya ya madaraka wakati akiongoza shirika hilo ambapo anakabiliwa na mashtaka manne ya kutumia madaraka vibaya na moja la kuisababishia Serikali hasara ya Sh887.1 milioni.

Hatua hiyo ilifikiwa leo mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Huruma Shaidi baada ya wakili wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), Leonard Swai kuieleza Mahakama kuwa wamekwisha wasilisha majumuisho yao ya mwisho mahakamani hapo.

Wakili wa Tido, Dk Ramadhani Maleta aliitaarifu Mahakama kuwa wakili mwenzake, Martin Matunda amefariki dunia na kwamba na wao pia wamekwisha wasilisha hoja zao za mwisho.

Baada ya kueleza hayo, wakili Swai aliiomba Mahakama kuipangia kesi hiyo tarehe ya hukumu na hakimu Shaidi akapanga kutoa hukumu Desemba 18.


from MPEKUZI

Comments