Akamatwa Akimfanyia Mdogo Wake Mtihani Wa Kidato Cha Pili.

Na John Walter, Manyara.
WATU wawili wanashikiliwa na jeshi la polisi mkoa wa Manyara kwa kosa la kufanya udanganyifu kwenye mtihani wa Kitaifa wa kidato cha pili.

Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake Kamanda wa polisi mkoani hapa Kamishna Msaidizi wa Polisi Augustino Senga alisema kuwa mitihani inaendelea vizuri isipokuwa  Novemba 12 mwaka huu lilitokea tukio moja la udanganyifu ambapo mwanafunzi ambaye tayari  amemaliza shule, aliamua kurudi shuleni kwa kushirikiana na  watumishi wa elimu wasio waaminifu.

Mwanafunzi huyo aliyemaliza masomo yake  aliweza kuingia darasani na  kufanya mtihani kwa kutumia jina la mdogo wake ambaye amekuwa mtoro  shuleni kwa kipindi kirefu kwa madhumuni ambayo anayajua yeye ama kuendelea na mafunzo ama elimu au kwa njia yoyote ili.

“Tukio hili llitokea  Novemba 12  mwaka huu ambapo Ofisa elimu kwa kushirikiana na polisi walipata taarifa kutoka kwa wasiri wetu kwamba kuna mwanafunzi ambaye ameingia kwenye chumba cha mtihani na hafahamiki na wale wanafunzi.

“Baada ya kufuatilia katika shule ya sekondari Qameyu iliyopo wilaya ya Babati mkoa wetu wa Manyara, kijana aitwaye Malkiad Massay mwenye miaka 18 alibainika akiwa katika chumba cha mtihani akifanya mtihani wa upimaji wa Kitaifa wa kidato cha pili huku akitumia jina la mwanafunzi aitwaye Martine Massay  wa kidato cha pili.

“Jina hili la kijana huyu amekuwa mtoro sana shuleni kwa kipindi kirefu na huyu mtuhumiwa Malkiad Massay ni kaka yake  wa baba mmoja na mama mmoja na kama nilivosema mwenye jina hilo amekuwa mtoro wa muda mrefu kwa hiyo kaka yake alitumia njia hiyo ya kuingia kwenye chumba cha mtihani ili aweze kufanya mtihani wa mdogo wake.

“Hii tunaamini walishirikiana na watendaji akiwepo mwalimu mkuu na watu wengine kwa sababu sio rahisi mwanafunzi akaingia pale bila kujua ambaye anajua mwanafunzi ni yupi anayetakiwa kufanya mtihani pale, kwa hiyo akawa amebainika akiwa ameshafanya mtihani mmoja ule wa kwanza.

“Basi kijana huyo amekamatwa lakini pia na mkuu wa shule hiyo anashikiliwa kwa mahojiano, mwalimu mkuu wa shule hiyo anaitwa Severine Umbaida mwenye miaka 58 ambaye pia ni mkazi wa Qameyu.

“Tukio hili ni la kufedhehesha ambalo  halina tija   kwenye elimu yetu na tunaamini katika uchunguzi wetu na wengine wote waliohusika na hili kwani hawa ni wa awali tu tutahakikisha tutawatia mbaroni na sheria itafuata mkondo wake.

“Tunataka watu wafanye mitihani kwa haki na kwa halali lakini  taarifa za awali zinaonyesha kwamba kijana huyu alishamaliza kidato cha nne na akafeli huko wilaya ya Mbulu mkoa hapa kwa hiyo alikuwa na nia ya kufanya mtihani huo labda apate kuendelea hapo ama mahali pengine na uchunguzi wetu utabaini kwa kadri tutakavoendelea na upelelezi”, Alieleza Kamanda Senga.


from MPEKUZI

Comments