Waziri wa Fedha:Marekebisho Ya Sheria Ya Takwimu Hayazuii Kufanya Tafiti

Na. WFM Mjini Bali Indonesia
Marekebisho ya Sheria ya Takwimu ya Mwaka 2018,  hayawazuii wadau wa takwimu kutoa takwimu  kwa ajili ya matumizi yao bali marekebisho hayo yanaweka  misingi ya kuzingatiwa wakati wa  utoaji wa takwimu hizo.

Hayo yameelezwa na Waziri wa Fedha na Mipango Dkt.  Philip Isdor Mpango, alipofanya mkutano na Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Fedha (IMF) anayewakilisha Tanzania na nchi nyingine (Africa Group 1 Constituency), Bw. Maxwell Mkwezalamba, katika Mikutano ya Benki ya Dunia (WB) na Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF) mjini Bali Indoneshia.

Dkt. Mpango amesema kuwa lengo la  marekebisho  ya sheria  hiyo ni  kurahisisha ufanyaji wa tafiti na utoaji wa matokeo ya tafiti na sio kuwabana wadau katika  ukusanyaji  wa   taarifa za kitakwimu  au kuzuia  mijadala ya  uchambuzi wa kisera wa matokeo ya takwimu rasmi.

“Tumekubaliana kutumia fursa  ya kuboresha Kanuni za Takwimu  kwa ajili ya kuweka mazingira ya utekelezaji  mzuri  wa   vipengele vya sheria  vilivyorekebishwa   kwa  kuwashirikisha wadau mbalimbali ili kuelewa lengo la marekebisho hayo”, alieleza Dkt. Mpango.

Marekebisho hayo ya kanuni za takwimu yatawezesha utekelezaji mzuri wa vifungu vya sheria vilivyorekebishwa ambapo ametoa wito kwa wadau kushiriki  katika mchakato wa marekebisho hayo.

Aidha, Waziri  alieleza kuwa mwezi Novemba mwaka huu Serikali itakutana na wadau wa maendeleo,  ili kutoa fursa kwa wadau hao kuelewa kwa kina  dhumuni la Serikali kufanya marekebisho yaliyofanyika na kupitishwa na Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mwezi Septemba 2018.

Vilevile, Waziri Mpango, alimueleza Mkurugenzi Mtendaji wa IMF kuwa marekebisho  makubwa ya kiuchumi ambayo yamefanywa na Serikali ya Awamu ya Tano yameambatana na mabadiliko ya  sheria  mbalimbali hususan  sheria za za madini kwa lengo la kuhakikisha rasilimali za nchi zinawanufaisha wananchi lakini pia wawekezaji wanaowekeza fedha zao nchini.

Aidha, alisema kuwa Bw. Kwezilamba, ni mwakilishi wa Tanzania kwenye Bodi ya Magavana wa IMF, hivyo ni muhimu aelewe maendeleo ya kiuchumi na kijamii yanayofanyika nchini Tanzania ili aweze kueleza uhalisia kwenye mikutano ya Bodi hiyo.

Naye Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT) Prof. Florens Luoga, alisema kuwa BoT imeendelea kuboresha Sera ya Fedha ya Mwaka 2017 ili kutatua changamoto za Sekta ya Fedha zinazoibuka zikiwemo za uhaba wa mikopo hasa katika Sekta binafsi.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Fedha (IMF) anaeiwakilisha Tanzania, Bw. Maxwell Mkwezelamba, aliipongeza Tanzania kwa hatua mbalimbali za maendeleo ya uchumi kwa kuwa imeendelea kuwa nchi inayopiga hatua kubwa ya maendeleo na kuwa mfano katika nchi za Afrika.

Ameishauri Tanzania kutumia ofisi yake ili Washirika wa Maendeleo waelewe dhumuni la marekebisho ya kiuchumi yanayoenda sambamba na maboresho ya sheria mbalimbali  ili  maendeleo hayo yawe endelevu.

Vilevile Dkt. Mpango, alifanya mkutano na Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Dunia (WB) anayewakilisha Tanzania na nchi nyingine (Africa Group 1 Constituency),  Bw. Andrew Bvumbe, wakati wa mikutano ya mwaka ya  WB na IMF inayofanyika mjini Bali Indonesia na kupongeza ushirikiano wa kimaendeleo na taasisi hizo.

Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano Serikali
Wizara ya Fedha na Mipango
Mjini Bali, Indonesia



from MPEKUZI

Comments