Profesa Lipumba Adai Mgombea Wa CUF Anahujumiwa Liwale, Amtaka Mkuu wa Mkoa Aache Kuwatisha Wanachama Wake

Profesa Ibrahim Lipumba, mwenyekiti wa CUF anayetambuliwa na Ofisi ya Msajili wa Vyama vya siasa amesema kuna njama za kukinyima ushindi chama hicho katika uchaguzi wa ubunge wa Liwale utakaofanyika Jumapili Oktoba 13, 2018.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Jumanne Oktoba 9, 2018, Lipumba amesema Liwale ni ngome ya CUF lakini wameanza kunusa harufu ya kupokwa ushindi.

“Mgombea wetu Mohamed Rashidi Mtesa anakubalika na tangu achaguliwe kuwa diwani kata ya Liwale amefanya mengi na hata kushirikiana na watendaji wa Serikali ila kwa sasa  tumeanza kuhisi kufanyiwa rafu, tunaiomba tume (Tume ya Taifa ya Uchaguzi-NEC)  itende haki," amesema Lipumba.

Amesema katika kudhihirisha kuwa Liwale ni ngome ya chama hicho, katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015, CUF ilishinda kata 17 na CCM kata saba.

Amedai kuwa CCM inataka kulichukua jimbo hilo kwa nguvu kwa kuwatumia baadhi ya watumishi wa umma.

Amesema si vyema Taifa wakati likiadhimisha kumbukumbu ya miaka 19  ya kifo cha Mwalimu Julius Nyerere, likaingia kwenye vurugu za uchaguzi Liwale.

“Tufanye uchaguzi wa haki ili mshindi apatikane kwa haki. Liwale ni ngome yetu na hiyo inatokana na mizizi iliyowekwa na muasisi  wa chama chetu Mzee Shaban Mloo.

"Mawakala wetu wamekula viapo lakini mpaka sasa hakuna hata mmoja aliyepewa nakala za viapo hii ni dhahiri kwamba kuna njama ambazo zinafanyika kutowapitisha ili wajitangazie ushindi kwa kuiba kura"

"Tunamtaka Mkuu wa Mkoa wa Lindi aache mara moja tabia ya kufanya mikutano ya hadhara kwa madai anahamasisha maendeleo na kuwataja wanachama wa CUF kuwa atawakamata kwa sababu yeye ni Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama " Amesema Prof Ibrahim Lipumba

Uchaguzi Liwale unafanyika baada ya aliyekuwa mbunge wa jimbo hilo kwa tiketi ya CUF, Zuberi Kuchauka kujiuzulu na kujiunga na CCM. Kuchakua ni mgombea wa CCM katika uchaguzi huo.


from MPEKUZI

Comments