Msemaji wa Simba Haji Manara Afunguka Sakata la Mo Dewji Kutekwa

Msemaji wa klabu ya soka ya Simba ambayo Mo Dewji ni mmoja wa wenye hisa,Haji Manara, amesema kwamba amezungumza na familia ya Mo Dewji na kuwataka wanasimba watulie, kwani wana amini atapatikana akiwa salama.

Manara amesema kwamba familia yake imemuahidi kuwa watulivu na kuwataka mashabiki wa Simba na wapenzi wa soka wote kutulia katika kipindi hiki ambacho vyombo vya usalama vinafanya kazi yake.

"Tumestuka sana, wengine tulipata taarifa mapema, nashukuru Jeshi la Polisi na kamati ya ulinzi na usalama chini ya RC Makonda, tunalowaomba wapenzi wanachama wa Simba watulie, familia yake wameniahidi kuwa watulivu, nimezungumza na mzee wake na familia yake katika hali ya utulivu, kwa hiyo tuwaombe watu watulie tuwaachie vyombo vifanye kazi yake, tunaloamini Mo atapatikana akiwa mzima Inshallah kwa uwezo wa Mwenyezi Mungu na watekaji watakamatwa", amesema Haji Manara.

Sambamba na hilo Haji Manara amewataka watu kutoa taarifa zozote kwa Jeshi la Polisi na sio kuzungumza kiholela, ili kulisaidia jeshi hilo kufanya kazi ya kumtafuta mfanyabiashara huyo.

Mo Dewji ambaye ni mmwekezaji na shabiki mkubwa wa timu ya Simba, ametekwa na watu ambao wametajwa kuwa ni wazungu asubuhi ya leo alipokuwa akienda gym.


from MPEKUZI

Comments