LHRC Wapinga Matumizi ya neno "HUO NI UMAMA" Kwa Madai Kwamba Linawadhalilisha Wanawake

Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), kimepinga vikali matumizi ya neno 'umama' katika mitandao ya kijamii kwa kile kilichodaiwa kuwa ni ubaguzi na udhalilishaji.

Tamko lililotolewa na kituo hicho limesema kuwa kwa kufanya hivyo neno hilo linahalalisha kuwa mwanamke ni kiumbe dhaifu, kwani mambo yanayofanywa na wanaume hata wanawake wanaweza kufanya pia.

"Mfano kuna hii sentensi, 'mwanaume kulea mtoto ni umama, mwanaume ni kubebesha mimba' kitu ambacho kinalenga ni udhalilishaji hivyo basi, kwa pamoja tuwajibike kupinga udhalilishaji kwa wanawake", imesema taarifa hiyo.

Neno 'umama' limeibuka siku za hivi karibuni katika mitandao ya kijamii, likijikita katika kuelezea namna ambavyo mwanaume anatakiwa kufanya vitu tofauti na wanawake kwa kutaja baadhi ya vitu ambavyo wanawake hawapaswi kuvifanya, jambo ambalo halina ukweli wowote.

Mbali na LHRC, mwingine ambaye amepingana na matumizi ya neno hilo ni Wakili msomi, Albert Msando ambaye alionesha kukerwa na msemo huo na kuandika maneno haya katika ukurasa wake wa Instagram,

"Aliyeanzisha huu utani (meme) wa ‘umama’ na wanaondelea nao nadhani wanasahau kwamba kama sio mama zetu basi tusingekuwa hapa tulipo. Ni upuuzi ni sentensi ambayo inamdhalilisha mwanamke. Kabla hujatunga sentensi na kutaka iwe ‘meme’ basi jiulize kama unaona aibu mama yako kuwa mama, utani huu unaonyesha ni jinsi gani bado ‘wanaume’ wanajiona wao ni bora kuliko wanawake".


from MPEKUZI

Comments