Atiwa Mbaroni Kwa Kumkata Panga na Kumuua Mtoto wa Mkewe Walie Achana Naye

Jeshi la polisi mkoani Mtwara linamshikilia mkazi wa Mkalapa wilayani Masasi kwa tuhuma za mauaji ya mtoto Clara Thomas (2) ambaye ni mtoto wa aliyewahi kuwa mke wake kwa kumkata  panga shingoni.

Akizungumza leo Jumamosi Septemba 15 mwaka huu, kamanda wa polisi Mkoa wa Mtwara, Lucas Mkondya amesema tukio hilo lilitokea jana(Ijumaa) katika Kijiji cha Chibwini baada ya mama mzazi wa marehemu kwenda kumtembelea mama wa mtuhumiwa ili kuwasalimia watoto aliowaacha kwa mwanaume huyo.

“Mtuhumiwa amezaa na mama wa marehemu watoto wawili na baada ya hapo wakaachana, lakini huyu mwanamke, alikwenda Msumbiji na kuolewa kisha kumzaa Clara (marehemu),”amesema Mkondya.

Kamanda Mkondya amesema baada ya mama kukaa muda mrefu Msumbiji  alifunga safari kuja Masasi kwa ajili ya kuwasalimia watoto nyumbani kwa mkwewe wa zamani.

“Wakati mama wa marehemu anafika nyumbani hapo, (mtuhumiwa)  alikuwa shambani lakini alirudi nyumbani baada ya kupata taarifa  kuwa mzazi mwenzake amefika kuwasalimu watoto,” amesema Kamanda.

Kamanda Mkondya ameeleza kuwa, wakati Clara anakwenda nyuma ya nyumba kujisaidia, mtuhumiwa  alimfuata nyuma na kumkata panga shingoni.

Amesema polisi wanakamilisha upelelezi na utakapokamilika watamfikisha mahakamni.


from MPEKUZI

Comments