Makamu Wa Rais Kumuwakilisha Rais Magufuli Katika Mkutano Wa SADC Nchini Namibia

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan anaondoka nchini leo kuelekea Windhoek, Namibia kushiriki kwenye Mkutano wa 38 wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (38th Ordinary Summit of SADC Heads of State and Government) unaotarajiwa kufanyika tarehe 17 na 18 Agosti, mwaka huu akimwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli.

Mkutano huo utakaofanyika chini ya Uenyekiti wa Namibia, utatanguliwa na Mikutano mingine mitatu ambayo ni Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali  wa Organ Troika, Mkutano wa Baraza la Mawaziri  na Mkutano wa Makatibu Wakuu.  

Aidha, Mkutano huo utapokea na kujadili agenda mbalimbali ikiwemo Uchaguzi wa Mwenyekiti na Makamu Mwenyekiti wa SADC, Uchaguzi wa Mwenyekiti na Makamu Mwenyekiti wa Asasi ya SADC ya Ushirikiano wa Siasa, Ulinzi na Usalama, taarifa ya Mwenyekiti anayeondoka wa SADC Organ, taarifa ya Katibu Mtendaji wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika, hali ya kiuchumi katika kanda ya SADC na taarifa kuhusu utekelezaji wa Kaulimbiu ya Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa mwaka 2017.

Vilevile, Mkutano utapokea  Kaulimbiu ya Mkutano wa 38 wa Wakuu wa Nchi na Serikali   na kupokea taarifa ya hali ya utekelezaji wa Mpango Mkakati wa Maendeleo ya Viwanda wa SADC. Katika Mkutano huo, Tanzania inategemea kuteuliwa kuwa Makamu Mwenyekiti wa SADC kwa kipindi cha Agosti 2018 hadi Agosti 2019.

Imetolewa na:
Ofisi ya Makamu wa Rais
Dar es salaam
15/8/2018


from MPEKUZI

Comments