IGP Sirro Apongeza hali ya Utulivu Uchaguzi Mdogo wa Marudio

Na Jeshi la Polisi.
Jeshi la Polisi nchini limewahakikishia wananchi kuendelea kuwepo kwa hali ya usalama na Amani hapa nchini ikiwa ni pamoja na kuendelea kuwepo kwa hali ya utulivu na usalama katika chaguzi ndogo.

Kauli hiyo imetolewa na Mkuu wa Jeshi la Polisi IGP Simon Sirro mjini Moshi Mkoani Kilimanjaro wakati akiwa katika ziara katika Shule ya Polisi Moshi (CCP) ambapo aliweza kuzungumza na Wakufunzi na Askari waliopo mafunzoni Chuoni hapo ikiwa na lengo la kukagua mwenendo wa mafunzo yanayoendelea katika Vyuo vya Polisi nchini.

IGP Sirro amesema katika maeneo yaliyofanya uchaguzi mdogo hali ilikuwa shwari licha ya kuwepo kwa matukio madogo ambayo yanaendelea kushungulikiwa na upelelezi utakapokamilika majalada yao yatapelekwa kwa Waendesha mashtaka kwa hatua zaidi.

“ Hali ilikuwa shwari na ni wazi kuwa wananchi sasa wameelewa umuhimu wa kutii sheria bila ya  kushurutishwa na natoa rai waendelee kudumisha hali hiyo ikiwa ni pamoja na kutoa taarifa za Wahalifu na uhalifu katika maeneo yao” Alisema Sirro.

Katika hatua nyingine akiwa Shule ya Polisi Moshi zamani CCP  IGP Sirro alitoa pongezi zake kwa Walimu na Uongozi kwa kazi kubwa wanayofanya ya kuwapika Askari hususani katika mafunzo yao ya awali ambapo ametaka kila Askari kutambua wajibu wake

Kwa upande wake Mkuu wa Shule ya Polisi Moshi Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP) Ramadhani Mungi amesema Chuo hicho kinaendelea kutoa mafunzo kwa umakini mkubwa ili kuhakikisha kuwa kila Askari anayetoka anakuwa na ukakamavu wa kutosha na nidhamu ya kuwahudumia Wananchi licha ya kuwepo kwa Changamoto za madeni ya maji na umeme.

Alisema wanaendelea kuboresha miundombinu ya Chuo hicho kwa kutumia miradi iliyopo ili kukiweka katika hali ya usalama zaidi ikiwemo kujenga uzio imara kuzunguka maeneo hayo.


from MPEKUZI

Comments